
Watu wengi wanatokea kusahau kufanya usafi wa kinywa na meno wakiamini kuwa hakuna tatizo litawapata katika kipindi cha mfungo. Kuhakikisha usafi wa kinywa na meno utasaidia kupunguza harufu mbaya ya kinywa na kinywa kuwa kikavu.
NINI HUTOKEA UKIWA UMEFUNGA?
Kufunga husababisha kuongezeka kwa kampaundi za madini ya sulphur katika kinywa na husababisha harufu mbaya ya kinywa. Watu wengi wanaamini kuwa kufunga husaidia kutibu magonjwa ya fizi, hii sio kweli. Kuongezeka kwa kampaundi za madini ya sulphur huenda sambamba na kupungua kwa mtiririko wa mate katika kinywa ambayo husababisha kutengenezwa kwa matabaka ya uchafu katika meno kitu ambacho moja kwa moja hupelekea matatizo ya fizi na meno kutoboka.
JINSI YA KUTUNZA AFYA YA KINYWA NA MENO KIPINDI CHA MFUNGO.
Changamoto nyingi za afya ya kinywa na meno huwepo kipindi cha mfungo. Wengi wamezoea harufu mbaya ya kinywa katika kipindi cha mfungo na huwa wanahisi ni jambo la kawaida. Fanya mambo yafuatayo ili kuimarisha afya yako ya kinywa na meno;
- Sukutua mdomo kuzuia harufu mbaya ya kinywa. Ingawa inakatazwa kumeza chochote kipindi cha masaa ya mfungo, ila unaweza kusukutua mdomo na kuhakikisha unatema kila kitu bila kumeza. Hii husaidia kuondoa ukavu wa mdomo na kuzuia meno kutoboka. Baada ya msaa ya mfungo hakikisha unakunywa maji au juisi za matunda. Epuka vinywaji vyenye caffein na chumvi kwa kuwa husababisha ukavu wa mdomo.

- Safisha meno kwa dawa ya meno yenye flouride kila baada ya masaa ya mfungo. Hii husaidia kuondoa tabaka la vyakula ambalo huwa na bakteria wanaosababisha meno kutoboka.

- Fanya uangalizi wa kinywa mara kwa mara. Inashauriwa kufanya uangalizi wa kinywa kabla ya mfungo haujaanza na mara baada ya mfungo kuisha ili kuhakikisha kama kuna tatizo lolote basi linatatuliwa. Pia kama kuna huduma yoyote inayohitaji dharura basi ni vizuri ukamwona daktari wa meno ili kufanya huduma ya haraka.

- Lishe bora. Lishe bora ni muhimu kwa afya ya mwili. Vyakula vyenye sukari husababisha meno kuoza. Hivyo basi unapokua unafuturu hakikisha unakula chakula bora chenye virutubisho muhimu kwani kukosa virutubisho kuna madhara mengi kwa afya ya kinywa. Kunywa vimiminika vingi hasa maji na kula matunda ili kuimarisha afya ya kinywa.

- Punguza ulaji wa Vyakula vinavyonata. Baada ya masaa ya mfungo, watu wengi hupenda kula vyakula vyenye kunata na sukari nyingi kama tende, chocolate na kadhalika. Vyakula hivi hunasa kwenye meno na huwa ni ngumu kuvitoa. hiyo husababisha meno kuoza na matatizo mengi ya kinywa. Hivyo basi unashauriwa kupunguza ulaji wa vyakula hivi ili kupunguza uuwezekano wa meno kuoza.

Mfungo ni kipindi muhimu sana katika maisha yetu, ingawa huwa tunatokea kusahau vitu vidogo kama afya ya kinywa na meno. Afya mbaya ya kinywa huleta madhara kwa mwili mzima, matatizo ya meno huleta shida wakati wa kula. Kusukutua, kupiga mswaki na kula chakula au lishe bora husaidia kuimarisha afya ya kinywa na meno. Kumbuka kumuona daktari wa meno kabla haujaanza mfungo na baada ya mfungo kuisha ili kuhakikisha afya ya kinywa na meno ipo imara. Muone daktari kila uhisipo maumivu na wakati wa dharura.
Comments
Post a Comment