KUOZA KWA JINO NI NINI?
Kuoza kwa jino ni kuharibika kwa jino ambako hutokea pale vijidudu au bakteria waliopo mdomoni wanapotengeneza kemikali (asidi) ambayo huharibu jino na kusababisha vijishimo kwenye jino. Vishimo hivyo visipotibiwa vinaweza kusababisha maambukizi (infection), maumivu hata kupotea kwa jino.
Jino lina matabaka makuu matatu
Tabaka la nje ambalo huitwa enameli (enamel)
Tabaka la kati liitwalo dentini (dentin)
Tabaka la ndani liitwalo fofota/tishu (pulp)
Matabaka mengi yakiharibika ndivyo tatizo linapokua kubwa zaidi.
NINI HUSABABISHA MENO KUOZA?
Vijidudu/bakteria na vyakula vyenye asili ya sukari vinaweza kusababisha meno kuoza. Kuna tabaka lenye mnato ambalo huwa linatengenezwa kwenye meno na fizi ambalo kwa kitaalamu huitwa "plaque". Tabaka hili huwa linahifadhi vijidudu au bakteria ambao hutumia sukari kama chakula chao. Bakteria wakiwa wanatumia sukari kama chakula chao hutengeneza kemikali (asidi), asidi hiyo ndiyo inayoshambulia meno na kuyafanya yatoboke. Mchakato huu wote hutokea dakika 20 au zaidi baada ya kula chakula chenye sukari.
Vitu ambavyo vinaweza kuchangia upate kutoboka kwa meno yako ni;
Kutosafisha meno mara kwa mara angalau mara mbili kwa siku na kutomwona daktari wa meno mara kwa mara angalau mara moja kwa kila miezi sita kwa ajili ya usafi wa kinywa na matibabu.
Kutumia vyakula vyenye sukari mara kwa mara ambavyo bakteria hutumia kama chakula na kuzalisha asidi ambayo husababisha meno kuoza.

Kutopata madini ya floridi kwa kiasi cha kutosha. Floridi husaidia kuzuia kuoza kwa meno kwa kuyafanya imara dhidi ya asidi inayotengenezwa na bakteria. Tunaipata floridi ya kutosha katika dawa za meno zenye viwango vilivyothibitishwa na wataalamu wa afya ya meno
Kutokuwa na mate ya kutosha kinywani. Mate husaidia kusafisha asidi itengenezwayo na bakteria. Kuna magonjwa ambayo husababisha uzalishwaji mdogo wa mate, ni vyema kuonana na wataalamu kwa ushauri na msaada zaidi hasa kwa watu wenye midomo mikavu.

Ugonjwa wa kisukari
Uvutaji wa sigara



Comments
Post a Comment