Ukiwa na mafua na au kikohozi, kuweka mwili wako sawa na katika hali ya usafi ni jambo la msingi na muhimu na hii inahusisha usafi wa kinywa pia. Zifuatazo ni njia rahisi ambazo unaweza kuzitumia ili kuhakikisha afya ya kinywa na meno inabaki kuwa nzuri na imara wakati unaumwa.
Ukiwa unaumwa mafua na kikohozi ni vyema kuziba mdomo na pua wakati wa kukohoa na kupiga chafya pia usisahau kuhakikisha afya ya kinywa chako inazingatiwa. Tafiti zinaonesha kwamba virusi vya mafua vina uwezo wa kukaa sehemu yenye unyevu kwa takribani masaa 72. Hivyo basi ni vyema kutoshirikiana kutumia mswaki mmoja kwa watu wawili pia ni vizuri kubadilisha mswaki mara baada ya kupona mafua ingawa asilimia za kupata mafua kutoka kwenye mswaki ni ndogo lakini ni vyema kuchukua tahadhari.
- Tumia dawa ambazo hazina sukari
Kama inavyojulikana kwamba sukari ndio chanzo kikubwa cha meno kuoza, hivyo basi kutumia dawa ambazo zina sukari zinaweza kuleta athari kwenye meno na kusababisha kuoza. Inashauriwa kutumia dawa ambazo hazina sukari na kila ukinunua dawa hakikisha unasoma label na kujua kwamba haina sukari.
- Sukutua na kutema baada ya kutapika
Moja ya athari za mafua kwa baadhi ya watu ni kutapika. Unapotapika, tindikali iliyopo tumboni huja mdomoni na kusambaa kwenye meno. Ikikaa kwa muda inaweza ikasababisha kulika kwa meno hivyo basi inashauriwa kusukutua baada ya kutapika na kupiga mswaki nusu saa baada ya kutapika ili kuhakikisha tindikali yote imekwisha kwenye meno.
- Kunywa maji mengi kujikinga na ukavu wa mdomo
Ukiwa unaumwa unahitaji kunywa maji mengi kwa sababu nyingi ikiwemo kuzuia ukavu wa mdomo. Ukavu wa mdomo unachangia sana katika kusababisha meno kutoboka pia dawa za mafua nyingi husababisha kinywa kuwa kikavu hivyo basi inashauriwa kunywa maji mengi kuhakikisha mtiririko wa mate unabaki vizuri.
Linapokuja suala la afya ya kinywa na mwili kwa ujumla, kinywaji kimoja huwa ndicho sahihi nacho ni MAJI. Ni vyema kuweka tabia ya kunywa maji ya kutosha kila siku. Vinywaji vingine sio mbaya kuvinywa lakini ni vyema kuhakikisha havina sukari. Wakati ambao unaumwa mafua na kikohozi muda mwingine unaweza kuwa unahitaji kitu cha moto ka ma chai, ni vyema kutotumia sukari nyingi na limao ambayo huwa ina madhara katika meno.
Comments
Post a Comment